Sunzu awashangaa Samatta, Ulimwengu
BEKI wa timu ya Taifa ya Zambia na TP Mazembe, Stopila Sunzu ameshangwa na
kitendo cha washambuliaji wa kimataifa wa Tanzania wanaocheza timu ya TP
Mazembe, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu kushindwa kujiunga na timu ya
Taifa.
Akizungumza na Mwananchi jana, Dar es Salaam, Sunzu alisema timu ya taifa
ndiyo daraja la mafanikio kwa mchezaji yoyote duniani kwa sababu, ubora wa
mchezaji hupimwa kwa mambo mengi na mojawapo ni mchango wake kwenye timu ya
taifa kwa mechi za kirafiki na mashindano.
“Hata mimi nilitegemea kukutana nao katika mechi hii, lakini sifahamu
kwanini hawajacheza labda ni majeruhi ndiyo maana wameshindwa kucheza,”
alisema.
Aliongeza: “Kama hawakuwa majeruhi watakuwa wamefanya makosa makubwa kwa
sababu mechi kama hizi zinafuatiliwa na watu wengi sana ikiwemo Shirikisho la
Soka Afrika (CUF).”
Kuhusu suala la nidhamu ya wachezaji hao Sunzu alisema kwamba wakiwa TP
Mazembe ni watu wenye nidhamu nzuri na wanajituma kwenye mazoezi na hata kwenye
mechi ndiyo maana wanapata namba.
“Moja ya sera muhimu ya TP ni nidhamu kabla ya uwezo wa mchezaji na ukikosa
nidhamu unaweza kukosa namba.”
Akizungumzia suala la majeruhi, alisema wakati wanaagana Congo DRC,
hakufahamu kama wachezaji hao ni majeruhi. “Kuna wakati mchezaji anaweza akawa
majeruhi, lakini akajikaza kutokana na umuhimu wake kwenye timu na umuhimu wa
mechi,” anasema.
Naye Kocha Mkuu wa timu ya Taifa, Kim Poulsen amesema kuwa wachezaji
wasiokuwa na moyo wa kuichezea timu ya Taifa hawatapata nafasi hata kama
watakuwa na uwezo kiasi gani.
Kim alisema hayo mara baada ya kuombwa kutoa maoni yake kufuatia Samatta na
Ulimwengu kuzomewa na mashabiki wakati wa mechi ya kirafiki ya kimataifa kati
ya Taifa Stars na Chipolopolo ya kwenye Uwanja wa Taifa Jumamosi.
Kocha huyo raia wa Denmark alisema hana maoni kuhusiana na suala la kuzomewa
kwa Samatta na Ulimwengu, ambao mara kwa mara wanakutana na vipingamizi
wanapoitwa kuichezea timu ya taifa.
“Sitaki kuwasemea mashabiki kuhusiana na suala hilo, lakini wao wanajua nini
walichokifanya, ila nimeweka utaratibu mwingine wa kufanya kazi.
Sihitaji mchezaji asiyekuwa na moyo na timu,” alisema Kim.
Sihitaji mchezaji asiyekuwa na moyo na timu,” alisema Kim.
Alisema kuwa anajua itachukua muda ili kuweza kupata timu imara, lakini
katika mpira wa miguu ni jambo la kawaida kwani hata wapinzani wao (Zambia)
wana historia hiyo mpaka kufikia mafanikio.
“Nnawapongeza wote. Tulikuwa na wakati mgumu hasa upande wa washambuliaji
ambapo ilinibidi kutumia viungo wengi ili kuweza kumiliki mpira na kushambulia
kwa kushtukiza, tuliweza kutengeneza nafasi nyingi na kutumia moja, hii ni
faraja kwangu na kwa Watanzania wote,” alisema.
Alisema kuwa matokeo ya mechi ya juzi ni makubwa kwa Tanzania, kwani
kuifunga timu bingwa katika Bara la Afrika ni jambo la kujivunia. “Hii ni
zawadi ya Krismass na Mwaka Mpya kwa wadau wa soka.”
No comments:
Post a Comment